
Msanii Chrispin Mangala maarufu kama Big Pin. Picha/ Kwa hisani.
Msanii Crispin Mangala maarufu kama Big Pin kwa mara ya kwanza amefichua kuwa alikesha na maiti ya msanii mwezake Issah Wangui Mmari maarufu kama E- Sir.
Big Pin amefichua kuwa ilimbidi kufanya hivyo wakati E-sir alipoaga dunia katika ajali kutokana na uchungu mwingi aliohisi.
“Nilikesha nikimtazama nikitumaini ataamka tuwe pamoja tena,” amesema Big Pin.
Wawili hao walikuwa kama chanda na pete na walianza mziki pamoja katika studio za Ogopa.
Katika mahojiano ya kipekee na Richard Njau maarufu kama Astar msanii huyo amedokeza kuwa yeye na E-sir walifanya kila kitu pamoja na kuondoka kwake kulikuwa pigo kubwa ambalo bado hajaweza kulistahamili kufikia sasa.
Big Pin kwa sasa anawika na kibao Ginene, huku akisema kuwa ataangusha kibao alichofanya na Nyashnski pamoja na Nameless hivi karibuni.
Msanii E- Sir alivuma na vibao Boomba Train, Sare, Sitishiki, Mossmoss.
Taarifa na Dominick Mwambui.